Monday, November 14, 2011

ZIARA YA MO KATIKA MRADI WA UBORESHAJI WA HUDUMA ZA MAJI SAFI NA SALAMA SINGIDA MJINI!


Mkurugenzi wa Mamlaka ya maji safi na taka Singida, SUWASA, Marin Churi akifafanua jambo kwa ugeni ulioambatana na Mbunge wa Singida Mjini,Mohammed Dewji (kushoto) kwenye msafara huo wakiwemo viongozi wa siasa.
Mkurugenzi wa SUWASA,Injinia Isaack Nyalonji Akitoa maelezo ya kisima kikubwa cha mradi wa BADEA katika eneo la Mwankoko, kushoto kwake Mbunge Mo Dewji alipotembelea kukagua mradi huo ambao unatarajia kumalizika Julai mwakani. Wa pili kushoto, Mstahiki Meya, Shehe Salum Mahami, eneo la chanzo cha mradi huo wa maji.
Mo Dewji akipata maelezo ya sehemu mbalimbali ndani ya eneo la Ujenzi la mradi wa Tanki kubwa na la kisasa kutoka kwa mmoja wa wataalum wa kampuni ya Spencon Service Ltd alipotembelea huko eneo la Mandewa.
Mo Dewji akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi mbalimbali mara baada ya kumaliza kukagua ujenzi wa mradi huo wa BADEA ambao unatarajiwa kumalizika Julai mwakani.
Moja ya Tanki la maji ambalo litakua likipokea maji na kusambaza sehemu nyingine mbalimbali. Mradi huu unajengwa na wataalamu kutoka kampuni ya Spencon Service Ltd. (Picha zote na Mo blog team).


Na Mwandishi Wetu.
Mbunge wa jimbo la Singida mjini, Mohammed Dewji amesema ataendelea kuhakisha anapigania kumaliza tatizo la maji kwenye jimbo hilo ikiwemo kupambana nalo mpaka ngazi ya juu wakiwemo wanaokwamisha mradi huo.


Dewji alisema hayo mapema leo wakati alipotembelea mradi wa uboreshaji wa huduma za Maji Safi na Salama Singida Mjini unaofadhiliwa na Benki yaMaendeleo ya Kiarabu (BADEA), Serikali na mashirika mengine yakiwemo Shirika la Mafuta ulimwenguni (OFID) unaogharimu dola za kimarekani bilioni 17.2(SHILINGI 25,800,000,000,00) mpaka kukamilika kwa mradi huo.


Alisema kua,mradi huo ambao ulianza kuombwa tokea miaka 10 iliyopita na kuja kukubaliwa mwaka 2009, umekumbwa na changamoto mbalimbali hali iliyopelekea kushindwa kukamilika kwa wakati hivyo kuahidi kuonana na viongozi wa juu akiwemo Waziri mwenye dhamana na Rais ilikuondoa tatizo lililokuwepo.


“Nimepokea taarifa kutoka kwa Mamlaka ya Maji Singida (SUWASA) na kudai kuwa miongoni mwa changamoto hizo kwa mradi huo ni kupita kwenye sehemu za hifadhi ya barabara na katika makazi ya watu, suala hili nitalishughulikia kuona tunafika wapi ikiwemo kuonana na waziri mwenye dhamana” alisema Dewji.


Kwa upande wake Injiania Isaack Nyakonji wa SUWASA alisema mbali na matatizo ya mradi huo kupita kwenye hifadhi ya barabara na makazi ya watu, pia hali ya ukame na tatizo la umeme limechangia kusuaua kwa mradi huo.


“Singida ndani ya miaka miwili tulikuwa na ukame sambamba na ukatikaji wa umeme hali hiyo ilipelekea mradi huu kusimama. Pia mabadiliko ya gharama ya mradi huu yameongezeka kutokana na mazingira kuwa magumu” alisema Eng.Nyakonji.


Katika ziara hiyo, Dewji alitembelea sehemu mbalimbali ya mradi huo maarufu kama BADEA na kujionea utendaji wa kazi ikiwemo eneo la visima Mwankoko na sehemu ya tanki kubwa na la kisasa ambalo likikamilika litasaidia kupunguza shida ya maji Singida Mjini.

No comments:

Post a Comment