Thursday, June 30, 2011

DKT. MOHAMMED GHARIB BILAL AKUTANA NA BALOZI WA VIETNAM NCHINI


Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Mohammed Gharib Bilal, akipokea zawadi ya picha kutoka kwa Balozi wa Vietnam nchini Tanzania, Nguyen Duy Thien, wakati alipomtembelea ofisini kwake Ikulu jijini Dar es Salaam, leo Jumatano Juni 29, 2011. Picha na Muhidin Sufiani-OMR
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania leo Jumatano Juni 29, 2011 ametembelewa na Balozi Nguyen Duy Thien wa Vietnam nchini Tanzania ofisini kwake Ikulu jijini Dar es Salaam. Balozi Thien pamoja na kufikisha salamu za watu wa Vietnam kwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pia alimueleza Makamu wa Rais kuwa anayo furaha kuwapo hapa Tanzania ambapo sasa ametimiza miaka miwili kufuatia Tanzania kuwa nchi yenye amani na utulivu.

Pia alifafanua kuwa uhusiano uliopo kati ya Tanzania na Vietnam ni wa kihistoria tangu wakati wa kupigania uhuru na nchi yake imekuwa ikiithamini Tanzania kama nchi rafiki ambayo wanaitazama sana katika uhusiano zaidi hasa katika sekta za uchumi.

Kwa upande wake Makamu wa Rais Dkt. Bilal alimueleza Balozi Thien kuwa Vietnam kama ilivyo Tanzania imepitia mapambano kadhaa ya kihistoria lakini akaishukuru serikali ya Vietnam kwa kupiga hatua hasa katika kilimo. “Natambua katika eneo la kilimo tunaweza kushirikiana kwa ukaribu, najua kwa upande wenu mmefanya vema hadi kuitoa nchi yenu katika nchi za chini kwa umaskini jambo ambalo na sisi tunapigana nalo kwa nguvu zetu zote,” alisema Makamu wa Rais Dkt. Bilal.


Balozi Thien alimuomba Makamu wa Rais kutazama namna Tanzania na Vietnam zinavyoweza kutanua ushirikiano hasa katika kuagiza na kuuza mchele ili kuwafanya wafanyabiashara wa Vietnam kuleta nafaka nchini bila kupitia kwa madalali, jambo ambalo Makamu wa Rais alilipokea na kumuahidi Balozi Thien kuwa atalifikisha kwa wahusika serikalini ili watazame namna njema ya kulifanyia kazi.

Kwa mwaka huu wafanyabiashara wa Vietnam wanashiriki kwa mara ya kwanza katika maonyesho ya Sabasaba wakiwa na banda lao. Vietnam imefanikiwa kutanua uchumi wake kwa kasi licha ya kuwa sasa inakabiliwa na kushuka thamani kwa fedha yake na kwa mujibu wa Balozi wa nchi hiyo, hali hii inatokana na kutokuwa na nishati ya kutosha sambamba na hali mbaya katika soko la dunia.

Kwa upande wa Tanzania eneo ambalo linabakia kuwa funzo na linaloweza kuchangia kukuza uhusiano kati ya Tanzania na Vietnam ni sekta ya kilimo na pia nchi hizi mbili zina historia ya uhusiano tangu wakati wa ukoloni.

No comments:

Post a Comment