Thursday, February 23, 2012

MAHAKAMA YATAIFISHA MELI YA MV TAWARIQ 1, CAPTAIN WAKE NA WAKALA WAHUKUMIWA KWENDA JELA MIAKA 20!

Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, leo imetoa hukumu dhidi ya raia watano wa China waliokuwa wakikabiliwa na kesi ya uvuvi haramu katika ukanda wa Tanzania maarufu kama ‘Kesi ya Samaki wa Magufuli’ na kuamuru serikali kuitafisha meli ya Tawariq 1 (One) waliyokuwa wakiitumia.



Akisoma hukumu hiyo Jaji AUGUSTINE MWARIJA amesema kwa kuzingatia hoja za wakili wa serikali na za upande wa utetezi ameamua kuitaifisha meli hiyo kwa manufaa ya umma ili kuzuia vitendo vya uvuvi haramu katika ukanda wa Tanzania.


Kuhusiana na hukumu ya washitakiwa, Katika shitaka la kwanza Jaji MWARIJA amewahukumu mshitakiwa wa kwanza ambaye alikuwa nahodha wa meli hiyo HSU CHIN TAI na wakala wa meli hiyo ZHAO HANGUING kulipa faini ya Shilingi Bilioni Moja au kutumikia kifungo cha miaka 20 jela kila mmoja.
Katika shitaka la pili, Mahakama Kuu pia imemtia hatiani nahodha CHIN TAI kwa kuongoza meli isiyotambulika na kumuhukumu kwenda jela miaka 10 au kulipa faini ya shilingi Milioni 20. Hata hivyo washitakiwa wameruhusiwa kukata rufaa.


Watuhumiwa wengine watatu HSU SHANG PAO, CA’ DONG LI na CHEN RUI HAI ambao walikuwa wanatetewa na mawakili wa kujitegemea IBRAHIM BENDERA na JOHN MAPINDUZI wameachiwa huru baada ya mahakama hiyo kuwaona hawana kesi ya kujibu.

No comments:

Post a Comment