Tuesday, January 3, 2012

VODACOM ILIPOWALILIA WANAHABARI MAREHEMU HALIMA MCHUKA NA JOHN NGAHYOMA!.


Mkurugenzi wa kituo cha Radio cha Sport FM cha Dodoma, Abdallah Majura akitoa pole kwa wafiwa wakati  wa mazishi.Hapa Rais Jakaya Kikwete akipeana mkono na Mkurugenzi Mkuu wa TBC Bw Clement Mshana wakati wa kutoa heshima za mwisho kwa mtangazaji Halim Mchuka leo katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili, kabla ya kwwenda kuzikwa makaburi ya Msasani baada ya Sala ya Ijumaa.

Kampuni ya simu ya mawasiliano ya Vodacom imepokea kwa mshtuko na huzuni kubwa taarifa za vifo vya wanahabari nguli nchini Bi. Halima Mchuka na Bw. John Ngahyoma. Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana, wanahabari hao wamefariki kwa siku tofauti akianza Halima juzi na baadae Ngahyoma aliyefariki asubuhi ya leo wote jijini Dar es salaam.
“Tunatoa mkono wa pole kwa familia za marehemu, waajiri wao na kipekee familia ya wanahabari nchini kwa kuondokewa na wapendwa wetu ambao walikuwa sehemu muhimu ya ujenzi wa tasnia ya habari na utangazaji nchini.”Alisema Ofisa Mkuu wa Masoko na Mahusiano wa Vodacom Tanzania Bi. Mwamvita Makamba
Marehemu Bi. Halima Mchuka alikuwa mtangazaji wa Shirika la Utangazaji Tanzania – TBC na Marehemu Bw. John Ngahyoma hadi umauti unamkuta alikuwa ni mwanahabari wa Shirika la Utangazaji la Uingereza – BBC Ofisi ya Tanzania.


Marehemu wote wawili watakumbukwa kwa jinsi ambavyo walikuwa mahiri katika tasnia ya habari na utangazaji kwamba mchango wao utaendelea kuwa chachu hasa kwa vizazi vijavyo vya wanahabari chipukizi nchini.


“Tutamkumbuka sana Marehemu Halima ambae rekodi zinaonyesha kuwa ni mtangazaji wa kwanza mwanamke kutangaza mpira. Marehemu Ngahyoma kwa upande wake ni sehemu ya watangazaji wa awali kabisa wa televisheni Tanzania Bara mwanzoni mwa miaka ya tisini”Alisema Mwamvita.


Mwamvita amesema kampuni ya Vodacom daima ina thamini na kuheshimu mchango wa wanahabari katika maendeleo ya taifa na ushamirishaji ustawi wa jamii.Mungu azilaze roho za Marehemu Bi Halima Mchuka na Bw. John Ngahyoma mahali pema peponi - Amen!

No comments:

Post a Comment