MATAIFA MBALIMBALI

                                           RAIS SALEH HUENDA HATARUDI YEMEN
 Afisa mmoja mwandamizi alisema atarudi nyumbani baada ya siku chache, lakini upinzani umeahidi kuwa watamzuwia, na kuna tetesi nyingi kuwa utawala wake wa miaka 30, pengine ndio umekwisha.
Vijana wengi walisherehekea katika Medani ya Chuo Kikuu cha Sanaa, na wengine walitoka barabarani wakipepea bendera.
Lakini milio ya bunduki na miripuko ilisikika.Piya kuna taarifa kutoka Taiz kuwa mapambano yamezuka, na watu kadha wameuwawa. Waliyemuona Rais Saleh Saudi Arabia, wanasema Rais Saleh aliteremka mwenyewe kwenye ndege lakini majaraha ya kichwani, usoni, na shingoni yakionekana.
Rais Ali Abdullah Saleh alijeruhiwa katika shambulio la kombora dhidi ya ikulu, ambapo rais na baadhi ya maafisa wake walijeruhiwa. Rais Saleh, akifuatana na jamaa zake, aliwasili Saudi Arabi usiku wa Jumamosi.
Lakini mwanawe wa kiume na mpwa wake, ambao wanaongoza jeshi, inaarifiwa wamebaki nchini, na hao ndio walioisaidia Marekani kupambana na ugaidi nchini Yemen. Rais Saleh alijeruhiwa chini ya moyo katika shambulio la kombora siku ya Ijumaa.
Maafisa wa serikali wamewalaumu watu wa makabila yenye silaha, wanaoshirikiana na wapinzani wa rais, kwa shambulio hilo, lakini makabila hayo yamekanusha kuwa yalihusika.
Mdadisi mmoja aliye karibu na Rais Saleh, anaona shambulio la Ijumaa lilitokana na bomu lilotegwa na mtu kati ya watu wanaomzunguka rais, lakini ni shida kuthibitisha hayo.
Swala ni jee, Rais Saleh, ambaye ameongoza nchi kwa miaka 33, ndiyo ameondoka kabisa, au atarudi?.